Sunday 30 September 2012

Mbowe afichua siri mgogoro wa RC, madiwani Moshi

MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman Mbowe, amesema mvutano uliopo kati ya madiwani wa Manispaa ya Moshi na Mkuu wa Mkoa (RC) wa Kilimanjaro ni mpango wa serikali kutotaka kuziachia halmashauri zinazoongozwa na chama hicho kufanya kazi zake mipango iliuyojiwekea.
Mbowe alisema kuruhusu wakuu wa serikali kupindisha maamuzi ambayo yamefanywa na vyombo hivyo vilivyopo kisheria, ni kujenga utawala wa kiimla katika taifa kwa kujiongoza kwa matamko au mapenzi ya viongozi badala ya kanuni za halmashauri.

Alisema kisheria Baraza la Madiwani linajiendesha kwa kanuni na sheria, kwa mamlaka walizopewa madiwani na wananchi, hivyo wakuu wa wilaya na mikoa wanapaswa kuviheshimu vikao hivyo na siyo kuruhusu kutumika na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuvuruga upinzani hata kwa kuvunja kanuni.


Mbowe ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Hai na Kiongozi wa Upinzani Bungeni, alisema mvutano uliopo sasa katika Baraza la Madiwani linaloongozwa na CHADEMA na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, ni ushuhuda mwingine wa matumizi yaliyovuka mipaka ya kimadaraka ambayo yamekuwa yakifanywa na wakuu wa wilaya na mikoa kuvuruga halmashauri zinazoongozwa na CHADEMA.


“Ndiyo maana sisi kama CHADEMA tunasema kuwa suluhu ya matatizo haya yote ni katiba mpya, kwani cheo cha mkuu wa mkoa na mkuu wa wilaya ni vyeo vya kufutilia mbali, kwanza mtu anayeteuliwa na rais hana maslahi yoyote kwa mwananchi badala yake ni kuwaingilia viongozi waliochaguliwa na wananchi kwa ajili ya kuvuruga amani na kushindwa kufanya kazi za maendeleo,” alisema Mbowe.


Alisema tatizo kubwa lipo kwa wakuu wa serikali kuruhusu kutumika na CCM ili kuleta chokochoko kwa mabaraza yanayoongozwa na CHADEMA, huku akitolea mfano mabaraza ya Hai, Arusha, Mwanza na Moshi ambapo kanuni zimekuwa zikivunjwa makusudi ili kusababisha madiwani waliochaguliwa na wananchi kushindwa kufanya kazi zao.


“Ukweli ni kwamba vikao vya halmashauri vipo kisheria na vinaweza kufanya maamuzi yake, lakini wakati mwingine vikao hivi vinaweza kuwa na madhaifu, hivyo ni vema mkuu wa mkoa na meya wakaitana mezani na kushauriana, kwani kuvutana kunakuwa hakuna mantiki yoyote.


“Kama ni matumizi mabaya ya fedha CCM imekwishafanya ubadhirifu mkubwa sana wa fedha ambao ulifanywa na viongozi tena wa chama hicho, najua huu ni mpango unaofanywa na CCM, lakini mimi Mbowe nasema CHADEMA itaendelea kujenga demokrasia ya haki kwa kuendelea kutamalaki kwa kupewa mamlaka na wananchi wenyewe, na siyo vinginevyo,” alisema Mbowe.


Mvutano uliopo kwenye Manispaa ya Moshi ni ule wa Mkuu wa Mkoa kuzuia safari ya madiwani, na watendaji kwenda Kigali Rwanda, safari ambayo ilikuwa igharimu sh milioni 123. Pia mkuu huyo alipingana na gharama hizo kwa kusema ni ndogo kwani itagharimu zaidi ya milioni 200.


Hata hivyo, Mbowe alisema kuwa kama madiwani wamekaa na kuona kuna umuhimu wa wao kufanya safari hiyo, ni vema mkuu wa mkoa angeheshimu maamuzi yao, kwani kama utaratibu huo ukiendelea madiwani waliochaguliwa na wananchi watashindwa kufanya maamuzi yao kwa kuongozwa na matamko kutoka kwa viongozi wa serikali.

No comments:

Post a Comment

Chadema UK Ndani ya Milton Keynes

DAR NI SISI - VIDEO MAISHA YA WANADAR HATA BAADA YA MIAKA50 YA UHURU