Monday 17 September 2012

CHADEMA kuanika ‘siri’ ya mauaji

VIJANA WAKE WASEMA SASA YATOSHA
BARAZA la Vijana wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (BAVICHA) leo linatarajiwa kuanika hadharani ukweli wa mauaji ya raia yanayodaiwa kufanywa na vyombo vya serikali katika mikoa kadhaa hapa nchini.

Kamati ya Utendaji ya BAVICHA, inayokutana mjini Morogoro, imesema itaweka wazi sintofahamu ya mauaji hayo yenye mwelekeo wa kisiasa bila uchunguzi huru kufanyika ili hatua stahili zichukuliwe kwa wahusika.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, BAVICHA imesema kuwa wamelazimika kufanya hivyo kwa kuwa inaamini haki ya kuishi hata kama ni ya raia mmoja, ina thamani kubwa kuliko kitu kingine chochote.

Bazara hilo limesema kuwa mauaji ya kada wao Mbwana Masudi, ambaye alitekwa na kuteswa mara baada ya uchaguzi mdogo wa jimbo la Igunda alikutwa ameuawa kikatili na watu ambao wanaaminika kuwa wafuasi wa CCM.

Wamesema hata baada ya uchaguzi wa Arumeru, kulikuwa na matukio mawili ya mauaji ambayo yote kwa namna moja yamehusishwa na siasa. Tukio la kwanza ni lile ambalo vijana watano walikutwa wameuawa huko Chekeleni, Arumeru, wakati tukio la pili ni lile lililomhusisha kiongozi wa CHADEMA, kata ya Arumeru, Msafiri Mbwambo, ambaye aliuawa kwa kuchinjwa.

Pamoja na kueleza vifo vya wanachama wake, BAVICHA walisema hawafurahishwi na kifo cha yeyote na ndiyo maana watatoa tamko hata la mauaji ya kijana katika kijiji cha Ndago, Iramba, mkoani Singida, aliyetajwa kuwa kiongozi wa UVCCM aliyekutwa amekufa katika mazingira ya kutatanisha ambayo yanahusishwa na siasa.

“Mauaji ya namna hiyohiyo yamefanyikwa hivi karibuni katika mkoa wa Morogoro ambako kijana mmoja, Ali Zona, aliuawa na polisi wakati jeshi hilo lilipovuruga mapokezi ya viongozi wa CHADEMA kwenda kwenye mkutano mkubwa wa hadhara.

Wamesema hali hiyohiyo imejirudia karibuni kabisa katika kijiji cha Nyololo, Iringa, ambapo mwandishi wa habari wa Channel Ten, Daud Mwangosi, aliuawa kikatili na kinyama na Jeshi la Polisi kwa kulipuliwa na kitu kinachodhaniwa kuwa ni bomu.

“Kwa namna yoyote ile Kamati ya Utendaji ya BAVICHA haiwezi kufumbia macho mauaji haya ambayo kwa kweli yana nia ya kudhibiti kasi ya mabadiliko ambayo watawala wanaiona kuwa inazidi kupamba moto.

Katika mauaji haya, hakuna hatua zozote za makusudi zilizochuliwa dhidi ya wale waliohusika na kikubwa serikali kupitia vyombo vyake imekuwa ikifanya mzaha katika kushughulikia jambo hili. Mauaji haya yanayotekelezwa na jeshi la polisi kwa amri za serikali ya CCM yamekuwa na dhamira moja tu ya kutaka kuupotosha umma kuwa CHADEMA ni chama cha fujo,” wamesema.

Waituhumu CCM kufadhili vijana wake

Katika hatua nyingine BAVICHA imekishukia Chama cha Mapinduzi kwa madai ya kufadhili vijana wake na kuwaweka kwenye makambi ambako wanafundishwa mbinu haramu za kudhuru raia wenzao ambao wanaonekana kuipinga hadharani.

Vijana hao wamesema wanao ushahidi wa kutosha unaodhihirisha kuwa mafunzo hayo yanatolewa na baadhi ya vyombo vya ulinzi na usalama vya nchi, kama ilivyofanywa kwenye makambi maeneo ya Irmaba, Singida, na Tabora wakati wa uchaguzi mdogo wa Igunga.

Aidha CCM imeendelea kutumia vijana kwa kuwakodi kutoka sehemu mbalimbali na kuwapeleka sehemu nyingine ya nchi kwa lengo la kutibua na kufanya fujo kwenye mikutano ya CHADEMA. Hali hii inathibitishwa na tukio la Ndago, mkoani Singida.

Askofu Mkuu Mtega avunja ukimya

Huko mjini Songea, mwandishi wetu Julius Konala, anaripoti kuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Songea Mhashamu Norbert Mtega amevitaka vyombo vya dola kuacha mchezo wa kutumia silaha kali hovyohovyo na kuchochea machafuko yanayowaumiza watu wasio na hatia.

Mhashamu Mtega alitoa kauli hiyo jana wakati wa sherehe za shirika la Mabinti wa Maria Imaculete DMI, na kuonya kuwa machafuko yanayozikumba nchi nyingi duniani, yalianza kwa mtindo unaoonekana kwa sasa hapa nchini.

Askofu Mtega bila kutaja tukio lolote, alisema madhara yanayoanza kuonekana nchini yamewagusa zaidi kina mama na watoto ambao hawana uwezo wa kujitetea na kuwafanya waangamie bila sababu za msingi.

“Nawaambieni kama tutaachilia mambo haya ya kutumia silaha hovyohovyo yakaendelea kwa kweli tutakuwa tunatafuta machafuko ambayo yatawaumiza watu wasiyo na hatia kabisa,” alisema.

Kauli ya Askofu Mtega inakuja siku chache baada ya kutokea kwa mauaji ya kikatili ya mwandishi wa habari wa kituo cha Runinga cha Channel Ten, Daud Mwangosi, mkoani Iringa, baada ya kupigwa bomu na askari polisi.

Mauaji ya Mwangosi ambayo yalitikisa nchi, yalitokea baada ya askari polisi kuvamia shughuli za ufunguzi wa ofisi za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), katika kijiji cha Nyololo, mkoani Iringa.

Hivi sasa, tume na kamati kadhaa zimeundwa kuchunguza sababu za mauaji hayo, ambapo jeshi la polisi limemfikisha mahakamani askari anayedaiwa kumuua mwandishi huyo wa habari.

Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment

Chadema UK Ndani ya Milton Keynes

DAR NI SISI - VIDEO MAISHA YA WANADAR HATA BAADA YA MIAKA50 YA UHURU