BARAZA la Vijana wa Chama
cha Demokrasia na Maendeleo (BAVICHA) leo linatarajiwa kuanika hadharani ukweli
wa mauaji ya raia yanayodaiwa kufanywa na vyombo vya serikali katika mikoa
kadhaa hapa nchini.
Kamati ya Utendaji ya
BAVICHA, inayokutana mjini Morogoro, imesema itaweka wazi sintofahamu ya mauaji
hayo yenye mwelekeo wa kisiasa bila uchunguzi huru kufanyika ili hatua stahili
zichukuliwe kwa wahusika.
Katika taarifa yake kwa
vyombo vya habari jana, BAVICHA imesema kuwa wamelazimika kufanya hivyo kwa kuwa
inaamini haki ya kuishi hata kama ni ya raia mmoja, ina thamani kubwa kuliko
kitu kingine chochote.
Bazara hilo limesema kuwa
mauaji ya kada wao Mbwana Masudi, ambaye alitekwa na kuteswa mara baada ya
uchaguzi mdogo wa jimbo la Igunda alikutwa ameuawa kikatili na watu ambao
wanaaminika kuwa wafuasi wa CCM.
Wamesema hata baada ya
uchaguzi wa Arumeru, kulikuwa na matukio mawili ya mauaji ambayo yote kwa namna
moja yamehusishwa na siasa. Tukio la kwanza ni lile ambalo vijana watano
walikutwa wameuawa huko Chekeleni, Arumeru, wakati tukio la pili ni lile
lililomhusisha kiongozi wa CHADEMA, kata ya Arumeru, Msafiri Mbwambo, ambaye
aliuawa kwa kuchinjwa.
Pamoja na kueleza vifo vya
wanachama wake, BAVICHA walisema hawafurahishwi na kifo cha yeyote na ndiyo
maana watatoa tamko hata la mauaji ya kijana katika kijiji cha Ndago, Iramba,
mkoani Singida, aliyetajwa kuwa kiongozi wa UVCCM aliyekutwa amekufa katika
mazingira ya kutatanisha ambayo yanahusishwa na siasa.
“Mauaji ya namna hiyohiyo
yamefanyikwa hivi karibuni katika mkoa wa Morogoro ambako kijana mmoja, Ali
Zona, aliuawa na polisi wakati jeshi hilo lilipovuruga mapokezi ya viongozi wa
CHADEMA kwenda kwenye mkutano mkubwa wa hadhara.
Wamesema hali hiyohiyo
imejirudia karibuni kabisa katika kijiji cha Nyololo, Iringa, ambapo mwandishi
wa habari wa Channel Ten, Daud Mwangosi, aliuawa kikatili na kinyama na Jeshi la
Polisi kwa kulipuliwa na kitu kinachodhaniwa kuwa ni bomu.
“Kwa namna yoyote ile
Kamati ya Utendaji ya BAVICHA haiwezi kufumbia macho mauaji haya ambayo kwa
kweli yana nia ya kudhibiti kasi ya mabadiliko ambayo watawala wanaiona kuwa
inazidi kupamba moto.
Katika mauaji haya, hakuna
hatua zozote za makusudi zilizochuliwa dhidi ya wale waliohusika na kikubwa
serikali kupitia vyombo vyake imekuwa ikifanya mzaha katika kushughulikia jambo
hili. Mauaji haya yanayotekelezwa na jeshi la polisi kwa amri za serikali ya CCM
yamekuwa na dhamira moja tu ya kutaka kuupotosha umma kuwa CHADEMA ni chama cha
fujo,” wamesema.
Waituhumu CCM kufadhili
vijana wake
Katika hatua nyingine
BAVICHA imekishukia Chama cha Mapinduzi kwa madai ya kufadhili vijana wake na
kuwaweka kwenye makambi ambako wanafundishwa mbinu haramu za kudhuru raia wenzao
ambao wanaonekana kuipinga hadharani.
Vijana hao wamesema wanao
ushahidi wa kutosha unaodhihirisha kuwa mafunzo hayo yanatolewa na baadhi ya
vyombo vya ulinzi na usalama vya nchi, kama ilivyofanywa kwenye makambi maeneo
ya Irmaba, Singida, na Tabora wakati wa uchaguzi mdogo wa Igunga.
Aidha CCM imeendelea
kutumia vijana kwa kuwakodi kutoka sehemu mbalimbali na kuwapeleka sehemu
nyingine ya nchi kwa lengo la kutibua na kufanya fujo kwenye mikutano ya
CHADEMA. Hali hii inathibitishwa na tukio la Ndago, mkoani Singida.
Askofu Mkuu Mtega avunja
ukimya
Huko mjini Songea,
mwandishi wetu Julius Konala, anaripoti kuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki
la Songea Mhashamu Norbert Mtega amevitaka vyombo vya dola kuacha mchezo wa
kutumia silaha kali hovyohovyo na kuchochea machafuko yanayowaumiza watu wasio
na hatia.
Mhashamu Mtega alitoa kauli
hiyo jana wakati wa sherehe za shirika la Mabinti wa Maria Imaculete DMI, na
kuonya kuwa machafuko yanayozikumba nchi nyingi duniani, yalianza kwa mtindo
unaoonekana kwa sasa hapa nchini.
Askofu Mtega bila kutaja
tukio lolote, alisema madhara yanayoanza kuonekana nchini yamewagusa zaidi kina
mama na watoto ambao hawana uwezo wa kujitetea na kuwafanya waangamie bila
sababu za msingi.
“Nawaambieni kama
tutaachilia mambo haya ya kutumia silaha hovyohovyo yakaendelea kwa kweli
tutakuwa tunatafuta machafuko ambayo yatawaumiza watu wasiyo na hatia kabisa,”
alisema.
Kauli ya Askofu Mtega
inakuja siku chache baada ya kutokea kwa mauaji ya kikatili ya mwandishi wa
habari wa kituo cha Runinga cha Channel Ten, Daud Mwangosi, mkoani Iringa, baada
ya kupigwa bomu na askari polisi.
Mauaji ya Mwangosi ambayo
yalitikisa nchi, yalitokea baada ya askari polisi kuvamia shughuli za ufunguzi
wa ofisi za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), katika kijiji cha
Nyololo, mkoani Iringa.
Hivi sasa, tume na kamati
kadhaa zimeundwa kuchunguza sababu za mauaji hayo, ambapo jeshi la polisi
limemfikisha mahakamani askari anayedaiwa kumuua mwandishi huyo wa
habari.
Tanzania
Daima
No comments:
Post a Comment