Thursday 20 September 2012

Chadema Wamlima Barua JK

WAMTAKA ACHUKUE HATUA DHIDI YA MAUAJI YA RAIA KINYUME CHAKE SERIKALI INAHUSIKA

 CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimemwandikia barua Rais Jakaya Kikwete kikimtaka achukue hatua dhidi ya matukio kadhaa ya mauaji ya raia yaliyotokea kwa nyakati tofauti katika mikutano yake ya hadhara kwenye Mikoa ya Singida, Tabora, Arusha, Morogoro, Iringa.
 
Hatua kilichopendeza ni pamoja na kuwawajibisha viongozi wenye dhamana; Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi, Mkuu wa Polisi, IGP Said Mwema; Mkuu wa Operesheni Maalumu Polisi, Paul Chagonja, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Michael Kamuhanda.
Barua hiyo ya Septemba 10, mwaka huu iliyoandikwa na Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe baada ya kikao cha Kamati Kuu ya chama hicho, imemtaka Rais Kikwete kuwafukuza kazi watendaji hao katika Serikali yake kwa kuwa wameshindwa kazi. Kimesema kwamba mauaji mengi miongoni mwa hayo, yametokea bila hatua stahiki za kisheria kuchukuliwa na kusema kwamba ukimya huo unaweza kutoa picha potofu kwa umma kwamba Serikali yake inaunga mkono au imewatuma polisi au watu wengine waliosababisha mauaji hayo.

Matukio ya vifo ambayo chama hicho kimetaka yachunguzwe ni pamoja na lile la Januari Mosi, mwaka jana mkoani Arusha, Igunga (Novemba, mwaka jana) na Arumeru Mashariki (Aprili, mwaka huu). Mengine ni lile la Iramba lililotokea Julai 14, mwaka huu, Morogoro (Agosti 27, mwaka huu) na Iringa Septemba 2, mwaka huu ambalo hata hivyo, shauri lake limeshafikishwa mahakamani. Kimedai kwamba katika Uchaguzi mdogo wa Arumeru Mashariki, Kiongozi wa Kata wa chama hicho, Msafiri Mbwambo alichinjwa huku chanzo cha kifo hicho kikielezwa kuwa ni masuala ya kisiasa.


Pia kilielezea mauaji yaliyotokea katika Kijiji cha Ndago, Wilaya ya Iramba, Singida na kudai kwamba kikundi cha watu kilivamia mkutano wa Chadema kwa mawe na kwamba licha ya polisi kuwapo eneo hilo, hawakuchukua hatua zozote. Chama hicho pia kimekumbusha mauaji ya mfuasi wake mkoani Morogoro, Ally Zona kikisema kifo hicho pia kina utata kwani taarifa ya polisi imesema alikufa kwa kugongwa na kitu kizito wakati chama hicho kikidhani kwamba alipigwa risasi.


Kimesema pamoja na matukio yote hayo, viongozi wote hao hawakuchukuliwa hatua zozote za kuwajibika kwa matukio hayo. Pia Chadema kimeonya kuwa hali hiyo ikiachwa inaweza kujenga dhana potofu kwa wananchi kuwa Jeshi la Polisi liko mikononi mwa CCM na kazi yake ni kulinda masilahi ya chama hicho kwa gharama yoyote ile jambo ambalo Mbowe alisema ikiwa Rais Kikwete atachukua hatua za kinidhamu dhidi ya viongozi hao, atakuwa ameudhihirishia umma kwamba Serikali yake haifumbii macho mauaji yanayofanywa na vyombo vya usalama nchini. Kimemtaka Rais Kikwete kuunda tume ya kijaji au kimahakama kuchunguza vifo vilivyotokea katika mikusanyiko, mikutano, maandamano au mazingira ya kisiasa yanayokihusisha Chadema.


Ikulu yajibu Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue alipoulizwa juu ya barua hiyo alisema haijafika ofisini kwake, huku akisisitiza kuwa kama imeandikwa kwa Rais si lazima ifike kwake.“Sijaiona, ila kama wamemwandikia Rais barua sidhani kama itakuja kwangu. Itakwenda kwake moja kwa moja,” alisema Balozi Sefue. Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye hakutaka kuzungumzia hatua hiyo ya Chadema akisema, “Siwezi kusema chochote kwa kuwa barua yenyewe sijaiona pia ni barua ya Rais.”Kauli ya Bavicha Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha), limemtaka Rais Kikwete kuunda tume huru yenye wataalamu wa sheria ili kuchunguza mauaji, utekaji, vurugu na unyanyasaji wa wananchi unaotokea kwenye mikutano ya siasa hasa inayokihusisha chama hicho.


Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Morogoro baada ya kikao cha baraza hilo taifa, Mwenyekiti wa Bavicha, John Heche alisema kwamba kama Rais Kikwete atashindwa kufanya hivyo, baraza lake kwa kutambua kuwa matukio mengi ya mauaji yamehusisha vijana, litahamasisha maandamano nchi nzima na kuishtaki Serikali yake.
 
Habari hii imeandikwa na Fidelis Butahe na George Njogopa, Dar na Hamida Sharif, Morogoro. www.mwananchi.co.tz

CHOPA NNE KUONGEZA NGUVU KATIKA AWAMU NYINGINE YA M4C

Ni awamu nyingine ya M4C
Zitashambulia mikoa minne
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kinakusudia kuendelea na Operesheni Sangara kwa nguvu kubwa ikiwemo kutumia helkopta nne na kuongeza idadi ya magari katika mikoa mbalimbali nchini kwa lengo la kuyafikia maeneo mengi ambayo miundombinu yake ni mibovu.

Chama hicho kitatumia helikopta hizo wiki mbili zijazo kitakapoendelea na operesheni hiyo yenye kauli mbiu ya Vuguvugu la Mabadiliko (M4C) katika Mkoa wa Iringa.

Operesheni hiyo ilitarajiwa kuanza mkoani Iringa Agosti 28, mwaka huu, lakini ilisitishwa baada ya chama hicho kukubaliana na Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Said Mwema, kwamba iendelee baada ya kumalizika kwa sensa ya watu na makazi.

Baada ya sensa kumalizika, Chadema kilitangaza kuisitisha operesheni hiyo kufuatia tukio la mauaji ya aliyekuwa mwandishi wa habari wa kituo cha televisheni cha Channel Ten, mkoani Iringa, Daudi Mwangosi kwa bomu wakati polisi wakikabiliana na wa wafuasi wa chama hicho kwenye ufunguzi wa tawi katika kijiji cha Nyololo katika wilaya ya mufindi, mkoani Iringa.

Akizungumza na waandishi wa habari mkoani Morogoro jana baada ya kumalizika kwa kikao cha Baraza la Vijana wa Chadema (Bavicha), Mwenyekiti wake, John Heche, alisema kuwa operesheni hiyo inatarajia kuanza tena ndani ya wiki mbili zijazo na itanzia mkoani Iringa na kuendelea katika mikoa mingine.

“Kwa taarifa yenu, sasa tutaruka angani na chopa nne kuongeza nguvu Operesheni Sangara, tutaendelea na Mkoa wa Iringa ambako tuliisimamisha kutokana na mauaji ya Mwangosi,” alisema Heche na kuongeza: “Tukitoka hapo tunapiga mikoa mingine.”

Heche alisema lengo la kutumia helikopta hizo nne ni kuwafikia wananchi wengi kuanzia ngazi ya kitongoji ili kuwaeleza mambo mbalimbali, yakiwemo maovu yanayofanyika nchini.

Mwenyekiti huyo wa Bavicha alisema hatua hiyo inatokana na baadhi ya sehemu katika wilaya mbalimbali na mikoa nchini kutofikika kwa njia ya gari kutokana na ubovu wa mindombinu ya barabara ambayo katika kipindi cha miaka 50 ya uhuru Serikali ya CCM imeshindwa kuiboresha.

Akizungumzia maazimio ya kikao cha kamati ya Utendaji cha Bavicha, alisema kuwa mstakabali wa vijana wa taifa hili hivi sasa unakabiliwa na na changamoto nyingi kutokana na serikali ya CCM kushindwa kusimamia mambo mbalimbali.

Alisema kutokana na hali hiyo, Kamati Tendaji ya Bavicha imeiagiza sekretarieti yake kuunda kikosi kazi au kamati ya kufanya utafiti zaidi ili kujua kwa kina matatizo ya vijana hususani kuanzia masuala ya kuporomoka kwa elimu, ukosefu wa ajira na kutoa ushauri juu ya mstakabali wa taifa baada ya mwaka 2015.

Heche alisema kuwa Bavicha itaendelea kuwaunga mkono walalahoi nchini, wakiwamo wamachinga na matatizo yanayowakabili wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu katika kupata mikopo yao pamoja na kuvifuatilia viwanda ambavyo vilikuwa vikitoa ajira mbalimbali na hivi sasa vimegeuka kuwa mabanda ya mifugo.

Mbali na maazimio hayo, pia baraza hilo limetoa tahadhari kwa vyombo vya dola na Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa, kuepusha kauli za vitisho zinazohatarisha amani ya nchi.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Bavicha Zanzibar, Sharifa Suleiman, alisema vurugu zote zinazotokea kwenye majukwaa ya kisiasa kwa sehemu kubwa zinatokana na propaganda zinazofanywa na CCM kwa lengo la kuichafua Chadema na kupendekeza kuwa ni muhimu CCM kikaondolewa kwenye orodha ya vyama vya siasa nchini.

“Tumeshuhudia wananchi wakiendelea kunyanyaswa na vyombo vyao vya dola wanavyovilipa kwa kodi zao,” alisema Sharifa.

Akifafanua zaidi alisema vyombo vya dola viondokane na mfumo wa kinyanyasaji wa kujichunguza vyenyewe na kulitaka Jeshi la Polisi kujisafisha kabla wanachi hawajaamka na kukataa kukandamizaji unaofanywa na baadhi ya askari wake bila kuchukuliwa hatua zozote.

Chadema ilianzia Operesheni Sangara katika Mkoa wa Morogoro na ilitarajia kuendelea nayo katika mikoa ya Iringa, Dodoma, Singida na Njombe.
CHANZO: NIPASHE

BAVICHA WALIA NA KIKWETE

BARAZA la Vijana la Chama cha Demokrasia na Maendeleo, BAVICHA, limemtaka Rais Jakaya Kikwete na serikali ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kuiepusha nchi katika machafuko kwa kuwawajibisha haraka viongozi wa dola katika Wizara ya Mambo ya Ndani kutokana na tuhuma za unyanyasaji, mateso na mauaji kwa raia wasio na hatia endapo wao hawataki kujitoa.

Waliotajwa wajiuzulu au wawajibishwe na Rais kwa maslahi ya umma ni Waziri wa Mambo ya Ndani Dk. Emanuel Nchimbi na Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini, IGP Saidi Mwema.

Aidha Mkuu wa Operesheni wa Jeshi la Polisi Paul Chagonja, kamanda wa polisi mkoa wa Morogoro, Faustin Shilogile, Kamanda wa Polisi mkoa wa Iringa, Michael Kamuhanda, na wakuu wa kikosi cha kutuliza ghasia mikoa hiyo wamependekeza washtakiwe.

Akisoma maazimio ya baraza hilo la taifa lililofanyika mjini hapa kwa siku tatu, Mwenyekiti wa BAVICHA Taifa, John Heche, alisema tayari serikali imeiweka nchi rehani kutokana na kufumbia macho matukio hayo yanayoendelea kufanywa na vyombo vya usalama.

“Mpaka sasa wananchi hawana imani na serikali yao hususan Jeshi la Polisi na haya matukio yameubadilisha ulimwengu jinsi polisi wanavyoendesha unyama kwa raia wasio na hatia kwa visingizio visivyo na maana,” alisema Heche.

Akifafanua juu maazimio 10 yaliyofikiwa na ya baraza hilo, Heche alisema kwa muda mrefu Jeshi la Polisi limekuwa likitumika kama kivuli cha Chama cha Mapinduzi kuficha uovu wake na lenyewe kujificha kwa chama hicho.

“Uone nchi hii inavyokwenda, huyu Kamuhanda aliua watu wanne Songea kumlinda kahamishiwa Iringa nako amefanya hayo hayo mpaka sasa hajakamatwa, huyo Shilogile aliua hapa Morogoro anafunikwafunikwa na hawa wote wamekuwa wakilindwa na makao makuu kupitia mkuu wa operesheni jeshi la polisi Paul Chagonja ambaye anaeneza uongo kwa umma kuwalinda polisi wenzie,” aliongeza.

Katika maazimio hayo likiwemo la kuwataka kujiuzulu, kuwajibishwa au kufunguliwa kosa la mauaji kwa mantiki ya ‘Common intention’ viongozi hao, BAVICHA pia lilimtaka Rais Kikwete kuunda tume huru ya kiuchunguzi ya kimahakama katika makosa yote yaliyotokea Arusha, Arumeru, Igunga, Ndago-Singida, Morogoro na Iringa.

Aidha baraza hilo linakusudia kuunda kikosi kitakachotafiti matatizo ya vijana likiwemo suala la elimu duni na ukosefu wa ajira na kutoa ushauri juu ya mustakabli wa taifa baada ya 2015, kuendelea kuwaunga mkono walalahoi nchini wakiwemo machinga, na imelaani CCM kuwatumia vijana katika mafunzo ya kijasusi kwani yanalenga kulichafua taifa.

Mbali na maazimio hayo pia baraza hili limetoa tahadhari kwa vyombo vya dola na Msajili wa Vyama vya Siasa John Tendwa kuepusha kauli za vitisho zinazohatarisha amani ya nchi huku wakimshauri kuifuta CCM kwa kufundisha ujasusi.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa BAVICHA Sharifa Suleiman alisema baraza limepitia na kuchambua kwa kina mustakabali wa kisiasa, vijana na sintofahamu iliyopo na inayozidi kudhihirika kuwa uongozi uliopo umeshindwa kuongoza hasa katika kusimamia rasilimali za nchi kwa faida ya Watanzania.

Tanzania Daima

Tuesday 18 September 2012

"Ni kuchagua baina ya kuwa kama Uingereza ama kuwa kama Zaire/Kongo." Mistari kutoka kwa Jenerali Ulimwengu

NI dhahiri kwamba nchi inaweza kuwa ndogo lakini watu wake wakawa wakubwa, wakati ambapo nchi inaweza kuwa kubwa na watu wake wakawa wadogo. Hapa nazungumzia nchi yenye ukubwa wa ardhi na ukubwa wa idadi ya watu. Wakati mwingine sifa hizi zinaweza pia kuambatana na nchi kuwa na rasilimali kubwa na nyingi za kutosha.
 
Ziko nchi kubwa kwa maana ya ukubwa wa ardhi na watu na pia rasilimali maridhawa, lakini ambazo watu wake wamebakia kuwa wadogo, na mataifa yaliyoundwa na watu hao yakawa ni madogo pia. Hizi ni jamii na nchi za watu wapuuzi. Nchi ambazo kwa ukubwa wa maili za mraba na ukubwa wa idadi ya watu ni ndogo lakini zikawa na watu wakubwa na mataifa yake yakawa makubwa ni nchi za watu walio makini.

Napenda kuvitaja vielelezo kadhaa vinavyodhirisha kiwango cha juu cha upuuzi ndani ya jamii au nchi ambayo inakuwa kubwa kwa eneo la maili za mraba, wingi wa watu na rasilimali kubwa. Mojawapo ya vielelezo vikubwa vya upuuzi unaoweza kufanywa na jamii au nchi ni pale nchi au jamii inaposhindwa kutumia rasilimali zake kwa manufaa ya watu wake na badala yake ikaziruhusu zikaendelea kuwanufaisha wageni wakati watu wake wanaendelea kudhalilika.

Aina hii ya nchi kimsingi ni nchi iliyokosa uongozi na ikawa inaendeshwa na watawala ambao ama hawana uwezo ama hawana utashi wa kuwaongoza watu wao kuelekea katika maendeleo ya kweli. Mara nyingi hawa ni watawala wanaotawaliwa na uroho wa utajiri binafsi na ambao muda wao mwingi watakuwa katika shughuli za kujikusanyia mali wasiweze kufikia masuala magumu ya maendeleo ya watu wao.

Aghalabu pia watawala wa aina hii watakuwa ni wapagazi wa mabwana wao kutoka nje, hawa wakiwa ni watu binafsi, serikali, makamupuni ya biashara na asasi za kiulinzi na kijasusi. Watawala wa aina hii wanawatumikia wageni na hawana haya kuonyesha hali hiyo. Ndio wale ambao kila wakishutumiwa kwa hili au lile wanakuwa wepesi kusema, “Mbona huko nje wanatushangilia?” Kana kwamba “huko nje’ ndiko kulikowachagua.

Mwisho wa siku watawala kama hawa hupoteza haiba (kama waliwahi kuwa nayo), huonekana zaidi wakijipendekeza kwa wageni, na huanza pole pole kuwaogopa watu wao kwa sababu hawana majibu kw maswali wanayoulizwa na watu wao ambao hawawezi kuelewa ufukukara wao unasababishwa na nin katika mazingira ya utajiri mkubwa. Na wala hawawezi kuelewa ubadhirifu unaofanywa na watawala ambao maelezo yao ya siku zote ni hali ngumu ya uchumi duniani.

Hawa ndio watawala wa nchi kama Zaire/Kongo niliowajadili majuzi, na ndio watawala wa nchi kama Nigeria. Zote hizi mbili ni nchi kubwa zenye watu wadogo zinaotawaliwa na watawala walafi. Haziwezi hata kidogo kuwa mataifa makubwa hata zingekuwa na utajiri mkubwa kiasi gani.

Nje ya bara la Afrika, ni nchi kama Urusi ambayo baada ya kusambaratika kwa himaya ya Sovieti (ambayo nayo ilikwisha kupoteza pumzi mapema) imekuwa ikijikokota chini kabisa ya utajiri ilio nao na uwezo wa watu wake. Leo Warusi ni watu wadogo, na taifa lao ni dogo likilinganishwa na ‘potensho’ yake. (Vijana wa Kenya waliimba: “Nchi ya kitu kidogo, nchi ya watu wadogo”).
Upande mwingine tunaona mataifa makubwa yaliyojengeka ndani ya nchi ndogo, kama Botswana na Mauritius, nchi zenye rasilimali kidogo lakini zenye uongozi makini ambazo zimeweza kuwafanya watu wake wawe wakubwa na watambulike hivyo duniani.

Katika historia ya dunia ya karne kadhaa zilizopita tunajifunza kwamba ‘kijinchi’ kama Uingereza, ambacho hakikuwa na lo lote wakati huo, kikiwa kimefungwa katika kisiwa ambacho kwa nusu ya mwaka kimeganda na barafu, kiliweza kutawala nusu ya dunia ya wakati ule na kuwaweka mamilioni ya wanadamu chini ya himaya yake kutoka mashariki hadi magharibi, kaskazini hadi kusini.
Ni jambo gani liliifanya Uingereza iweze kuitawala dunia, kutawala Bara Hindi pamoja na watu wengi wale, tena wenye mapokeo na utamaduni wa fahari? Ni nguvu ya kujiamini, kuamini katika uwezo mkubwa wa jamii na uongozi wake na kuamini katika uwezo usiotishika wala kutikisika mbele ya adui au mpinzani ye yote.

Imani hii katika uwezo wa Uingereza ilipandikizwa akilini na mioyoni mwa watoto wa Uingereza tangu wakiwa ‘nkeremeke’ (neno la Kihaya linalomaanisha kichanga) na imani ambayo walikuwa nayo ikawa ni silaha kubwa kila walikokwenda kupora nchi za watu wengine ili kuiletea fahari himaya ya Uingereza.
Hawakuendekeza watawala wala rushwa na wasaliti wa watu wao, na angalau mara moja mfalme wao alipodhihirika kutaka kuwakandamiza walizua uasi na wakamkamata na kumkata kichwa. Katika msukumo wa kutafuta fahari ya Uingereza hawakuvumilia upuuzi.

Mzee mmoja wa Uingereza aliyewahi kufanya kazi kama mtawala wa kikoloni nchini Tanganyika aliniambia kuwa siku ya kwanza shuleni walikusanywa kwenye gwaride la shule nzima na mkuu wa shule akawaambia: ‘Nyie watoto mna bahati kwani mmezaliwa mkiwa Waingereza. Hiyo ina maana mmeshinda bahati nasibu ya kwanza katika maisha yenu.”

Nani anaweza kuwaambia watoto wa Tanzania kitu kama hicho leo hii? Katika mazingira mengi watoto wanaweza hata kumzomea kwa sababu hawaoni ni nini hasa kiwafanye waone fahari ya kuwa Watanzania, watu wenye mashaka katika kila idara ya maisha yao, wanaoongozwa na watawala ambao wanaelekea bado wanatafuta kuelewa ni nini hasa maana ya uongozi?

Jamii au nchi inakuwa ya kipuuzi iwapo ina kila aina ya rasilimali lakini rasilimali hizo haziisaidii jamii wala nchi kuendelea wala kuwa jamii au nchi ya furaha. Furaha ndani ya jamii si lazima itokane na maendeleo makubwa ya kiuchumi na ujenzi wa vitu kama barabara na majumba. Hivi ni muhimu, lakini si kila kitu. Zipo jamii duniani ambazo kwa vigezo hivi zinaitwa jamii masikini, lakini viwango vyake vya furaha viko juu sana.

Hizi ni jamii ambazo zimeridhika na hali ya maisha kwa sababu zimeweza kujenga utangamano kati ya rasilimali zilizopo na mafanikio ya kimaisha ya watu wake. Mathalan, jamii inaingiza kipato cha shilingi kumi, kila mwanajamii analijua hilo, halafu jamii inanufaika kwa kiwango cha shilingi kumi, na kila mwanajamii analijua na kulielewa hilo, na wanajamii wote, isipokuwa mwendawazimu, wanaridhika.

Jamii inajihatarisha yenyewe iwapo itafanya kinyume cha hilo, iwapo, mathalan, itaingiza kipato cha shilingi kumi kisha ikaruhusu shilingi moja tu itumike kwa manufaa ya jamii halafu jamii isijue shilingi tisa zilizobaki zimetumika vipi. Hata kama hakuna wizi au ubadhirifu katika matumizi bado misingi ya vita itakuwa imekwisha kujengwa kutokana na nakisi ya taarifa, uwazi, uelewa na maridhiano.

Maridhiano ni tunda la maelewano na maelewano ni tunda la kueleweshana katika uwazi. Uwazi unapopungua na sehemu ya jamii ikahisi kwamba inadhulumiwa au haitendewi haki unakuwa ndio mwanzo wa chokochoko na mfarakano.

Uwezo wa kuchagua umo ndani yetu. Tunaweza kuchagua kuwa nchi kubwa kwa maana ya eneo la maili za mraba na idadi kubwa ya watu (na rasilimali nyingi na kubwa) lakini papo hapo tukawa taifa la wapuuzi, tukajulikana hivyo duniani, au tukachagua kuwa taifa dogo kwa vigezo vya ukubwa wa ardhi, idadi ya watu na rasilimali lakini tukatumia rasilimali hizo ndogo, udogo wa idadi ya watu wetu na udogo wa eneo la mraba la nchi yetu kuwa (na kutambulika kama) taifa kubwa.

Ni kuchagua baina ya kuwa kama Uingereza ama kuwa kama Zaire/Kongo
 
Jenerali Ulimwengu, Rai ya Ulimwengu, Raia mwema, Toleo la 257, 5 Sep 2012

 

MBUNGE WENJE AUTEKA MKUTANO WA PINDA

Mbunge wa Nyamagana (Chadema), Hezekiah Wenje, jana aliuteka mkutano uliopangwa kuhutubiwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambapo wananchi waliohudhuria walimshangilia zaidi yeye (Wenje) huku wakinyoosha vidole viwili ambayo ni alama ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Hali hiyo ilijiri jana saa 11:00 baada ya msafara wa Waziri Mkuu kuingia katika viwanja vya Sahara huku Wenje akiwa miongoni mwa waliofuatana na Pinda.

Baada ya Pinda kuteremka kwenye gari na kuanza kuelekea kwenye meza kuu huku akisalimiana na baadhi ya wananchi, sehemu kubwa ya umati uliokuwepo walikuwa wakionyesha ishara ya vidole viwili na mara walipomuona Wenje walilipuka kwa shangwe ambapo Mbunge huyo machachari naye aliwanyooshea ishara ya vidole viwili.

Kama vile haitoshi baada ya Waziri Mkuu na viongozi wa mkoa wa Mwanza aliokuwa amefuatana nao kuketi vitini, ndipo Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Baraka Konisaga, alisimama kwa ajili ya kufanya utambulisho na alianza kwa kumweleza Pinda kuwa hizo ndizo harakati za miji mikubwa.

Wakati Konisaga akisema hivyo, wananchi waliendelea kushangilia, hali iliyomfanya adai kuwa wanamshangilia yeye (Konisaga) kwa sababu ndiye mtawala wa eneo hilo, lakini wananchi walionekana kuguna kwa sauti kama ishara ya kutokubaliana naye.

“Hayo makofi mnanishangilia mimi, kwa sababu bila mimi hakuna mkutano,” alisema Konisaga na kupokelewa na sauti za wananchi walionekana kupingana naye wakisema weweeee! Katika utambulisho, Konisaga alianza kwa kumtambulisha Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza, Wilson Kabwe, lakini wananchi walionekana kupinga hatua hiyo ndipo Konisaga akawaambia bila yeye (Kabwe) hakuna maendeleo Mwanza.

Hatimaye Konisaga alimtambulisha Wenje ambaye alisimama kuelekea jukwaani huku akishangiliwa kwa nguvu na wananchi ambao walikuwa wakimshangilia kwa kuimba “mbunge, mbunge, mbunge”.

Alipofika jukwaani na kupewa kipaza sauti, Wenje alianza kwa kusema: “Mheshimiwa Waziri Mkuu, hili ndilo Jiji la Mwanza. Kwa kipindi cha miaka miwili iliyopita sijawahi kuona nguo za kijana uwanjani hapa.”

Kauli yake ilizididha mlipuko wa sauti za wananchi wakimshangilia na ndipo alianza kumweleza Waziri Mkuu kwamba Jiji la Mwanza lina malalamiko mengi ya wananchi kuhusu migogoro ya ardhi.

“Mheshimiwa Waziri Mkuu, Jiji la Mwanza lina malalamiko mengi ya ardhi. Nimesema sana ndani ya Bunge, lakini mnanijibu kisanii. Nimemweleza na Waziri wa Ardhi kwamba wanaoteseka sio Chadema peke yao kwani hata wana-CCM nao wana malalamiko vilevile,” alisema.

Wenje ambaye alikuwa amepewa nafasi ya kusalimia tu, aliongeza kuwa ni matumaini yake kwamba ujio wa Waziri Mkuu katika mkoa wa Mwanza utaleta ufumbuzi wa migogoro iliyokithiri katika sekta ya ardhi.

CHANZO: NIPASHE

PINDA AZOMEWA MWANZA, MKUTANO WAKE WANUSURIWA NA MBUNGE WENJE WA CHADEMA

VIJANA MWANZA WAIMBA ‘PEOPLE’S POWER, HATUITAKI CCM’

WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda, jana alijikuta katika wakati mgumu baada ya kushindwa kuhutubia maelfu ya wakazi wa Wilaya ya Nyamagana, jijini Mwanza kwa muda kutokana na wananchi wengi kumzomea.

Kiongozi huyo alikumbana na kisanga hicho cha aina yake akiwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mwanza, Clement Mabina pamoja na Mkuu wa Mkoa huo, Mhandisi Evarist Welle Ndikilo.

Pinda na viongozi hao, walikumbana na zomeazomea hiyo kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika viwanja vya Sahara jijini hapa, ikiwa ni hitimisho la ziara ya Waziri Mkuu huyo ya siku saba mkoani Mwanza.

Chanzo cha Pinda na viongozi hao kuzomewa mkutanoni hapo, ilitokana na kile kilichoonekana kuwepo kwa kero nyingi zilizodaiwa kushindwa kupatiwa ufumbuzi na Serikali ya CCM chini ya Rais Jakaya Kikwete.

Kitendo hicho cha wananchi kilimlazimisha Pinda kushindwa kuhutubia kwa muda, huku akionekana kujawa jazba.

Sababu nyingine ya wananchi kuzomea, ni hatua ya Pinda kuwaambia wananchi hao watoke mjini waende vijijini wakalime waachane na mambo ya upinzani wa kisiasa.

Pinda alitoa kauli hiyo baada ya kundi la vijana mkutanoni hapo kuonesha alama ya V, bendera ya CHADEMA na nyimbo za Peoples, Power.

Kwa mazingira hayo, askari wa polisi wa kikosi cha kutuliza ghasia (FFU), waliokuwa na silaha nzito za kivita aina ya SMG, mabomu na marungu waliokuwepo mkutanoni hapo, walianza kuwatishia kuwapiga wananchi hao kwa lengo la kumlinda kiongozi huyo.

Baada ya kuzidi zomeazomea hiyo, Waziri Mkuu, Pinda alilazimika kumuita mbunge wa Nyamagana, Ezekiel Wenje (CHADEMA), aliyekuwa meza kuu, kisha kusema: "Nyamazeni basi!. Wenje...hii ndiyo serikali ya siku chache zijazo. Kwa namna hii naona hamuwezi, maana itakuwa ni vurugu asubuhi hadi jioni". Akazomewa kisha wakaimba hatutaki CCM, hatutaki CCM. .

Baada ya kuona hivyo, Pinda akacheka na kusema: "Hahahaaaaa, hata mkiimba peoples power, CCM ndiyo inayowaongoza". Akazomewa tena kisha Pinda akashindwa kuendelea kuzungumza jukwaani.

Akahutubia mkutanoni hapo, Pinda aliwataka wananchi hao waache ushabiki wa kisiasa, na kwamba halmashauri ya jiji la Mwanza inayoongozwa na CHADEMA, ndiyo itapaswa kulaumiwa kama itashindwa kutekeleza miradi ya maendeleo kwa wananchi wake.

"Hapa jiji la Mwanza linaongozwa na CHADEMA. Meya wa CHADEMA, mwenyekiti wa Mipango miji wa CHADEMA, Naibu Meya ni wa CHADEMA. Lakini kama wameshindwa kuweka mipango mikakati ya kuwasaidia tutasema hawafai," alisema kisha akazomewa kwa mara nyingine.

Baada ya zomeazomea hiyo kuonekana kumwelemea Waziri Mkuu huyo, Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Ndikilo alilazimika kuingilia kati kwa kusema: "Wanaozomea tunawafahamu, na tunawafahamu waliowaleta hapa ili mje kufanya nini". Akazomewa.

Hata hivyo, baada ya hali kutulia kidogo, Pinda aliendelea kuhutubia huku akiwataka wananchi wa jiji la Mwanza waondoke mjini waende vijijini wakalime, jambo lililoonekana pia kuwakasirisha wananchi wengi kisha kumzomea tena.

Ingawa Pinda alilazimika kutumia muda mfupi kutoa hotuba yake, aliwaomba wana Mwanza washirikiane kuleta maendeleo yao, na kwamba iwapo tatizo ni Mkurugenzi wa jiji suala hilo litaangaliwa.

Aliwaomba wadumishe amani iliyopo hapa nchini, ikiwa ni pamoja na kushirikiana na Serikali kupambana na vitendo vya uvuvi haramu katika Ziwa Victoria, ili kuweza kuzua samaki wadogo wasivuliwe kisha kuharibu mazalia ya rasilimali hiyo.

"Jambo jingine ninalotaka kuwaeleza hapa leo ni hili la uvuvi haramu. Samaki ndani ya Ziwa Victoria wameisha...na hii ni kwa sababu ya uvuvi usiozingatia sheria. Tushirikianeni kupambana na vitendo hivi", alisema Pinda kisha akazomewa tepa.

Tanzania Daima

BAVICHA TAIFA WAKUTANA MOROGORO KUPANGA MIKAKATI YA KUIMARISHA CHAMA



John Heche , Septemba 17, 2012 alifungua Kikao cha Kamati ya Utendaji ya Bavicha kilichohudhuriwa na wajumbe kadhaa kutoka Mikoa yote ya Tanzania Bara na Visiwani.Kikao hicho kilipanga kujadili ajenda mbalimbali za Vijana na baadaye kufikia kutoa tamko la pampoja kuhusiana na masuala ya kisiasa, kijamii na kiuchumi.Hata hivyo katika Kikao hicho , Bavicha kupitia Mwenyekiti wake wa Taifa , walimkaribisha Mwandishi wa Habari na Mtangazani wa zamani wa TBC, Jerry Muro ili aweze kuwasalimia wa wajumbe wa Baraza hilo walioanza kukutana tangu Septamba 14 hadi 18, mwaka huu.Katika salaamu zake , Muro alisema, yenye ni mwanaharakati na mtu anayependa kusema ukweli, hivyo kwake mtu kama huyo ni lazima amuunge mkono kama ilivyo kwa vijana wa Bavicha wanavyosimamia kusema ukweli na kuamua kuwaunga mkono kwa hilo

Monday 17 September 2012

Mheshimiwa Ndesamburo akutana na Mwenyekiti Wa Chadema UK


CHADEMA kuanika ‘siri’ ya mauaji

VIJANA WAKE WASEMA SASA YATOSHA
BARAZA la Vijana wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (BAVICHA) leo linatarajiwa kuanika hadharani ukweli wa mauaji ya raia yanayodaiwa kufanywa na vyombo vya serikali katika mikoa kadhaa hapa nchini.

Kamati ya Utendaji ya BAVICHA, inayokutana mjini Morogoro, imesema itaweka wazi sintofahamu ya mauaji hayo yenye mwelekeo wa kisiasa bila uchunguzi huru kufanyika ili hatua stahili zichukuliwe kwa wahusika.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, BAVICHA imesema kuwa wamelazimika kufanya hivyo kwa kuwa inaamini haki ya kuishi hata kama ni ya raia mmoja, ina thamani kubwa kuliko kitu kingine chochote.

Bazara hilo limesema kuwa mauaji ya kada wao Mbwana Masudi, ambaye alitekwa na kuteswa mara baada ya uchaguzi mdogo wa jimbo la Igunda alikutwa ameuawa kikatili na watu ambao wanaaminika kuwa wafuasi wa CCM.

Wamesema hata baada ya uchaguzi wa Arumeru, kulikuwa na matukio mawili ya mauaji ambayo yote kwa namna moja yamehusishwa na siasa. Tukio la kwanza ni lile ambalo vijana watano walikutwa wameuawa huko Chekeleni, Arumeru, wakati tukio la pili ni lile lililomhusisha kiongozi wa CHADEMA, kata ya Arumeru, Msafiri Mbwambo, ambaye aliuawa kwa kuchinjwa.

Pamoja na kueleza vifo vya wanachama wake, BAVICHA walisema hawafurahishwi na kifo cha yeyote na ndiyo maana watatoa tamko hata la mauaji ya kijana katika kijiji cha Ndago, Iramba, mkoani Singida, aliyetajwa kuwa kiongozi wa UVCCM aliyekutwa amekufa katika mazingira ya kutatanisha ambayo yanahusishwa na siasa.

“Mauaji ya namna hiyohiyo yamefanyikwa hivi karibuni katika mkoa wa Morogoro ambako kijana mmoja, Ali Zona, aliuawa na polisi wakati jeshi hilo lilipovuruga mapokezi ya viongozi wa CHADEMA kwenda kwenye mkutano mkubwa wa hadhara.

Wamesema hali hiyohiyo imejirudia karibuni kabisa katika kijiji cha Nyololo, Iringa, ambapo mwandishi wa habari wa Channel Ten, Daud Mwangosi, aliuawa kikatili na kinyama na Jeshi la Polisi kwa kulipuliwa na kitu kinachodhaniwa kuwa ni bomu.

“Kwa namna yoyote ile Kamati ya Utendaji ya BAVICHA haiwezi kufumbia macho mauaji haya ambayo kwa kweli yana nia ya kudhibiti kasi ya mabadiliko ambayo watawala wanaiona kuwa inazidi kupamba moto.

Katika mauaji haya, hakuna hatua zozote za makusudi zilizochuliwa dhidi ya wale waliohusika na kikubwa serikali kupitia vyombo vyake imekuwa ikifanya mzaha katika kushughulikia jambo hili. Mauaji haya yanayotekelezwa na jeshi la polisi kwa amri za serikali ya CCM yamekuwa na dhamira moja tu ya kutaka kuupotosha umma kuwa CHADEMA ni chama cha fujo,” wamesema.

Waituhumu CCM kufadhili vijana wake

Katika hatua nyingine BAVICHA imekishukia Chama cha Mapinduzi kwa madai ya kufadhili vijana wake na kuwaweka kwenye makambi ambako wanafundishwa mbinu haramu za kudhuru raia wenzao ambao wanaonekana kuipinga hadharani.

Vijana hao wamesema wanao ushahidi wa kutosha unaodhihirisha kuwa mafunzo hayo yanatolewa na baadhi ya vyombo vya ulinzi na usalama vya nchi, kama ilivyofanywa kwenye makambi maeneo ya Irmaba, Singida, na Tabora wakati wa uchaguzi mdogo wa Igunga.

Aidha CCM imeendelea kutumia vijana kwa kuwakodi kutoka sehemu mbalimbali na kuwapeleka sehemu nyingine ya nchi kwa lengo la kutibua na kufanya fujo kwenye mikutano ya CHADEMA. Hali hii inathibitishwa na tukio la Ndago, mkoani Singida.

Askofu Mkuu Mtega avunja ukimya

Huko mjini Songea, mwandishi wetu Julius Konala, anaripoti kuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Songea Mhashamu Norbert Mtega amevitaka vyombo vya dola kuacha mchezo wa kutumia silaha kali hovyohovyo na kuchochea machafuko yanayowaumiza watu wasio na hatia.

Mhashamu Mtega alitoa kauli hiyo jana wakati wa sherehe za shirika la Mabinti wa Maria Imaculete DMI, na kuonya kuwa machafuko yanayozikumba nchi nyingi duniani, yalianza kwa mtindo unaoonekana kwa sasa hapa nchini.

Askofu Mtega bila kutaja tukio lolote, alisema madhara yanayoanza kuonekana nchini yamewagusa zaidi kina mama na watoto ambao hawana uwezo wa kujitetea na kuwafanya waangamie bila sababu za msingi.

“Nawaambieni kama tutaachilia mambo haya ya kutumia silaha hovyohovyo yakaendelea kwa kweli tutakuwa tunatafuta machafuko ambayo yatawaumiza watu wasiyo na hatia kabisa,” alisema.

Kauli ya Askofu Mtega inakuja siku chache baada ya kutokea kwa mauaji ya kikatili ya mwandishi wa habari wa kituo cha Runinga cha Channel Ten, Daud Mwangosi, mkoani Iringa, baada ya kupigwa bomu na askari polisi.

Mauaji ya Mwangosi ambayo yalitikisa nchi, yalitokea baada ya askari polisi kuvamia shughuli za ufunguzi wa ofisi za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), katika kijiji cha Nyololo, mkoani Iringa.

Hivi sasa, tume na kamati kadhaa zimeundwa kuchunguza sababu za mauaji hayo, ambapo jeshi la polisi limemfikisha mahakamani askari anayedaiwa kumuua mwandishi huyo wa habari.

Tanzania Daima

Mbunge: Mwenge wa uhuru marufuku , Adai ukifika jimboni kwake ataongoza kuuzima

MBUNGE wa Arumeru Mashariki, mkoani Arusha, kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Bw. Joshua Nassari, ameshikilia msimamo wa kupiga marufuku Mwenge wa Uhuru kufika jimboni kwake na kuwataka wananchi kuupuuza akidai hauna tija kwa maendeleo yao.

Aliwataka wananchi jimboni humo wakae mkao wa kula kwani jitihada za kuyatwaa mashamba makubwa yanayomilikiwa na wageni, zinaendelea hivyo wawe wavumilivu.

Bw. Nassari aliyasema hayo mwishoni mwa wiki katika mkutano wa hadhara wa Operesheni Sangara uliofanyika kwenye Kata ya Usa River, wilayani humo.

Aliwaataka wananchi kuupuuza mwenge huo, kutoshiriki kuchangia mchango wowote na kusisitiza kama mtu yeyote atabughudhiwa kutokana na ujio wa mwenge amualifu.

“Sioni sababu ya Mwenge wa Uhuru kukimbizwa maeneo mbalimbali nchini kwani badala ya kuhamasisha maendeleo, umegeuka sehemu ya ufujaji wa fedha za wananchi.

“Hali hii inachangia umaskini wa Taifa na kuhamasiha maovu katika maeneo yote ambayo mwengu huu unalala, nasema hivi, Mwenge wa Uhuru marufuku kufika jimboni kwangu.

“Mtu yeyote ambaye ataombwa mchango kwa ajili ya mwenge muiteni mwizi na mimi nitakuwa wa kwanza kuuzima baada ya kufika jimboni kwangu,” alisema Bw. Nassari.

Aliwataka wananchi hao kuendelea kushiriki shughuli za maendeleo bila kujali itikadi zao kisiasa na kuihadharisha Halmashauri ya Meru kuzingatia maadili ya utendaji kazi na kuacha kuwabughudhi wananchi kwa kuwachukulia bidhaa zao hasa wanapokusanya ushuru sokoni kupitia wakala wao.

Akizungumzia suala la uvamizi wa mashamba, Bw. Nassari
aliwataka wananchi kuwa wapole kwani anaandaa mkakati wa kuhakikisha ndani ya miaka mitatu, wamiliki wa mashamba hayo wanakimbia wenyewe ili wananchi waweze kujitwalia ardhi yao.

Katika hatua nyingine, Bw. Nassari alisema fedha zilizotengwa na halmashauri kwa maendeleo Kata ya Usa River, kuanzia Julai mosi mwaka huu hadi June mwaka 2013, ni sh. milioni 54.3 ambazo zitatumika kuboresha miundombinu na huduma ya maji safi.

Alisema ukarabati wa barabara kutoka Usa River hadi Magadilishu umetengewa sh. milioni nane na barabara za mji mdogo katika kata hiyo zenye urefu wa kilometa tano, zitagharimu sh. milioni 75.

Katika mkutano huo, wafuasi 15 kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM), na Tanzania Labour Party (TLP) walitangaza kuvihama vyao vyao na kujiunga CHADEMA.


Majira

Sunday 16 September 2012

TASWIRA MBALI MBALI ZA MKUTANO WA CHADEMA MILTON KEYNES

Engineer Prudence akishusha madongo mazito.

Mchungaji Mathew akimwaga sera.

Dr John Lusingu akitoa mifano hai

 Mwenyekiti wa Chadema-UK Chris Lukosi akihutubia

Kamanda Makelele, Katibu mwenezi wa moshi mjini aki wapa nasaha viongozi wa Chadema UK.

Brother Cobby akijiunga rasmi na Chadema.

Mzee Makelele akimkabidhi kadi mwanachama mpya dada AZIZA.

Mwenyekiti wa wanawake akiwahimiza akina mama kujiunga na M4C

Baadhi ya wanachama wapya kwenye picha ya pamoja na viongozi

Thursday 13 September 2012

CHADEMA yafungua kesi mahakamani dhidi ya Nape; Yazungumzia inakopata ufadhili

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimekiri kufadhiliwa kutoka nje ya nchi katika shughuli zake za kujijengea uwezo.

Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dkt. Willibrod Slaa alisema hayo jana katika semina iliyoshirikisha baadhi ya viongozi wa chama hicho na wageni kutoka shirika la Chama cha Kikristo cha Ujerumani (CDU) la Konrad Adenauer Stiftung (KAS).

Kwa mujibu wa Dkt. Slaa, CHADEMA na KAS, wamekuwa na ushirikiano wa karibu kwa miaka sita sasa na ushirikiano huo umelenga zaidi kukuza demokrasia nchini.

Dkt. Slaa alidai kuwa CHADEMA ni chama chenye uwazi kwa kila mtu na katika uhusiano wao na KAS, hakiletewi fedha moja kwa moja kwa ajili ya operesheni au maandamano, ila kujijenga kiuwezo.

“Kwa sasa kumekuwa na propaganda zinazoenezwa kwamba CHADEMA wanapata mabilioni ya fedha kutoka kwa wafadhili, hii si kweli, ila wanatujengea uwezo na si kutufadhili kampeni. Napenda kusema propaganda za aina hii zimepitwa na wakati na wote watakaozifanya tutawafungulia kesi,” alisema Dkt. Slaa.

“Wanaosema kwamba CHADEMA wanapokea mabilioni nao wanashirikiana na mashirika ya aina hiyo yenye mrengo mmoja na ni utamaduni duniani kote, vyama vyenye mrengo mmoja kushirikiana, hivyo hii dhana isipotoshwe,” alidai.

Pamoja na kusema kuwa KAS haitoi fedha moja kwa moja kwa CHADEMA kwa ajili ya maandamano na kampeni, lakini Dkt. Slaa alidai kuwa shirika hilo huwasaidia wastani wa Sh milioni 60 kwa mwaka kwa ajili ya machapisho na kutoa elimu.

Pia alisema kipo chama cha Uholanzi ambacho hakukitaja jina, lakini akakiri kuwa huwafadhili Sh milioni 20 kulingana na idadi ya wabunge walio bungeni.

Pamoja na kusema kuwa ni kawaida kwa vyama vya mrengo mmoja kusaidiana duniani, Dkt. Slaa alisema chama hicho cha Uholanzi kinachowasaidia, pia hufadhili CCM fedha zaidi ya zinazopelekwa CHADEMA kutokana na chama hicho tawala kuwa na idadi kubwa ya wabunge.

Nape ashitakiwa

Dkt. Slaa alidai kwamba kwa kuanzia wameamua kumshitaki Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye.

Kwa mujibu wa madai ya Dkt. Slaa, tayari CHADEMA imefungua kesi namba 186 ya mwaka 2012, katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam dhidi Nape, ambaye anadaiwa alitamka CHADEMA kufadhiliwa kutoka nje.

Dkt. Slaa alisema kuwa, kesi hiyo yenye tuhuma zaidi ya tano, pia itawaunganisha watu wengine waliowahi kutamka kauli za namna hiyo vikiwamo vyombo vya habari vilivyoandika taarifa hiyo.

“CHADEMA tumeamua kumfikisha Nape mahakamani, ili atuthibitishie hayo mamilioni tunayopokea kwa wafadhili wa Ujerumani na kesi hii, itawaunganisha na wale waliowahi kusema kauli kama hiyo. Hapa mnaona kuna wageni, hawa ni viongozi kutoka Ujerumani na baadhi yao ni watumishi wa Serikali ya nchi hiyo, sasa tumekutana hapa kwa makusudi, ili kuwaeleza wazi jinsi wenzetu wanavyosema kutokana na ushirikiano wetu na wao. Tunashangaa sana, yaani CHADEMA ikishirikiana na watu kutoka nje ya nchi wanasema na kuzusha mambo ambayo yanaweza kuleta utengano kati ya nchi na taifa jingine. Kwa mfano, sisi CHADEMA tunashirikiana na Taasisi ya Korrad Adenauer Stiftung ya Ujerumani, CCM inashirikiana na FES, CUF inashirikiana na FNF zote za Ujerumani, sasa tunataka Nape atueleze mbele ya Mahakama juu ya jambo hili,” alisema Dkt. Slaa.

Dkt. Slaa alidai kuwa kesi hiyo itakapokuwa ikiendelea, wataongeza watu wengine walioeneza kauli hiyo.

Semina ya KAS

Akizungumzia semina ya kujenga uwezo iliyotolewa jana kwa makada wa CHADEMA, Dkt. Slaa alisema imelenga kuangalia wanavyoweza kuleta uchumi wa soko utakaoshirikisha watu walio katika ngazi za juu na chini.

Lengo la kushirikisha watu hao wa tabaka mbalimbali kwa mujibu wa Dkt. Slaa, ni ili raslimali za nchi zitumike kwa faida ya Watanzania wote ambapo pia mgeni kutoka KAS ambaye alipata kuwa Naibu Waziri wa Uchumi na Maendeleo wa Ujerumani, Klaus-Jurgen Hedrich atatoa mada.

Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe alisema ili uchumi uwe endelevu, lazima wananchi wapewe haki na kuruhusu sekta binafsi kusimamia uchumi na si rahisi kusimamia uchumi kwa sera za kijamaa.

Mbowe pia alisema lengo la kukutana na mawaziri na wabunge wa Ujerumani jana ni kujadili masuala ya uchumi duniani na mahitaji yake katika nchi mbalimbali. Akasema chama cha siasa kinapaswa kutimiza majukumu yake, lakini pia kinapaswa kutambua kina wajibu wa kujadili uchumi wa taifa lake pamoja na utamaduni wa asili.

“Leo tumekutana na viongozi kutoka Ujerumani kubadilishana uwezo wa kisiasa, kujifunza kutengeneza vitabu, Katiba na mafunzo kwa viongozi. Lakini, nimetumia nafasi hii kuwaeleza hili la CCM na Serikali yake kutoa tuhuma kutufadhili jambo ambalo watalifanyia kazi kadiri watakavyoona. Pia tumewaeleza kwamba, Serikali hii inapokwenda kuomba msaada katika mataifa makubwa inasema inatekeleza sera na uchumi wa soko, lakini wanaporudi nyumbani wanawaeleza wananchi kuwa wanatekeleza ujamaa na kujitegemea jambo ambalo ni uongo. Sisi CHADEMA tupo pande zote, tunachagua yaliyo mazuri katika pande hizo na kuyafanyia kazi ili kuendana na soko huru, kuna misingi ambayo wakipewa watu binafsi wanaweza kusimamia uchumi, lakini hiyo isiondoe wajibu wa Serikali kutekeleza wajibu wake kwa wananchi,” alisema.

Naye aliyekuwa Mbunge na Waziri wa Uchumi na Maendeleo katika Serikali ya Ujerumani, Klaus-Jurgen Hedrich, alisema maendeleo ya nchi yoyote hayaji kama hakuna uhuru wa kutoa maoni na uhuru wakujitawala.

Alisema kwamba, ili wananchi wapate maendeleo ni lazima Serikali itoe fursa sawa ya kuwasikiliza wanachodai na kwamba, Tanzania inasifika kwa amani na utulivu lakini anashangaa kuwapo na malalamiko,” alisema.

Katika mazungumzo yake, alionyesha kutoridhishwa na kifo cha Mwandishi wa Habari wa Kituo cha Channel ten, Marehemu Daudi Mwangosi, aliyeuawa Iringa wakati akitekeleza wajibu wake.


Wavuti

MH. JOHN MNYIKA NA MAJIBU YA TANESCO KUHUSU UCHAFUZI WA MAZINGIRA NA FIDIA KWA WANANCHI WANAOISHI MAENEO HATARISHI YA KARIBU NA MITAMBO YA KUFUA UMEME UBUNGO




SIJARIDHIKA NA MAJIBU YA TANESCO KUHUSU UCHAFUZI WA MAZINGIRA, FIDIA YA WANANCHI WANAOISHI MAENEO HATARISHI YA KARIBU NA MITAMBO YA KUFUA UMEME UBUNGO IHARAKISHWE

 

Tarehe 9 Septemba 2012 baadhi ya vyombo vya habari viliandika habari kwamba wakazi zaidi ya 500 wa eneo la Ubungo Darajani karibu na Riverside wanalalamika kuishi kwenye mfereji wa maji taka wenye mafuta ya mitambo na mchanganyiko wa kemikali kadhaa zinazodaiwa kuzalishwa na Shirika la Umeme nchini (TANESCO).

Sijaridhika na majibu yaliyotolewa na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Felichism Mramba kwamba shirika hilo limedhibiti mfumo wa maji taka na haihusiki na tatizo hilo la kuchafua makazi na mazingira.
Kufuatia kauli hiyo, natoa wito kwa Wizara ya Nishati na Madini na TANESCO kutoa majibu ya wazi kwa wananchi ni kampuni gani hasa inahusika na uchafuzi huo wa mazingira na kuchukua hatua zinazostahili kurekebisha mfumo uliopo.

Ikiwa hatua hazitachukuliwa nitaungana na wananchi kufikisha malalamiko yao kwenye mamlaka zinazohusika na usimamizi wa mazingira katika Manispaa ya Kinondoni na katika Baraza la Usimamizi wa Mazingira (NEMC).

Waziri wa Nishati na Madini na Kaimu Mkurugenzi wa TANESCO watoe majibu ya wazi kwa wananchi ni lini fidia ya wananchi wanaoishi katika maeneo hatarishi yanayozunguka mitambo ya kuzalishia umeme ya Ubungo itaanza kulipwa katika mwaka wa fedha 2012/2013 kutokana na kiasi cha shilingi bilioni 10 ambacho tayari kimeshaingizwa kwenye bajeti.

Izingatiwe kwamba tarehe 04 Aprili 2012 nilifanya mkutano na wafanyabiashara ndogondogo maarufu kama wamachinga zaidi ya 500 katika kata ya Ubungo ambapo pamoja na mambo mengine nilitoa siku tatu kwa Wizara ya Nishati na Madini na TANESCO kueleza hatua walizochukua katika kutekeleza ahadi waliyoniahidi kwa nyakati mbalimbali kwenye mwaka wa fedha 2011/2012 wakati wa vikao vya kamati ya nishati na madini nilipohoji kuhusu hatma ya wananchi wanaoishi katika maeneo hatarishi jirani na mitambo ya umeme ikiwemo kuhusu uchafuzi wa mazingira unaoendelea.

Ikumbukwe kwamba mwaka 2004 baada ya mitambo kulipuka serikali iliahidi kuwalipa fidia wananchi husika na kuwahamisha, mwaka 2009 Serikali ikarudia tena ahadi hiyo lakini mpaka tarehe 4 Aprili 2012 ilikuwa haijatekelezwa hata kwa mtu mmoja.

Ndani ya siku hizo tatu, TANESCO ilitoa ahadi ya kuwa suala la fidia kwa wananchi litaingizwa katika bajeti ya serikali mapema iwezekanavyo na tayari kiasi cha shilingi bilioni 10 kimetengwa kwa ajili ya kuanza kulipa fidia ikiwa ni sehemu ya Mradi wa Kuboresha Mifumo ya Umeme Katika Jiji la Dar es salaam (Kasma 3154).

Ili kuhakikisha kwamba mpango wa kulipa fidia ikiwa ni sehemu pia ya kuboresha mazingira ya eneo husika tarehe 27 Julai 2012 katika hotuba yangu bungeni kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani niliitaka Wizara ya Nishati na Madini ieleze iwapo kiasi cha 10,000,000,000 kilichotengwa kwa ajili ya kulipa fidia wananchi wanaoishi katika maeneo hatarishi yanayozunguka mitambo ya kuzalishia umeme ya Ubungo kitatosha kukamilisha kazi hiyo kwa mwaka wa fedha 2012/2013 ili kuepusha uwezekano wa gharama kuongezeka kutokana na riba ya kuchelewa kufanya malipo kama ilivyotokea kwa miaka iliyopita.

John Mnyika (Mb)
09 Septemba 2012

Thursday 6 September 2012

CHADEMA waikataa tume ya Nchimbi

 TENDWA AIBUKA, ATISHIA KUWAFUTIA USAJILI
 
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimeipinga tume ya kuchunguza mauaji ya aliyekuwa mwandishi wa Channel Ten, Daudi Mwangosi, iliyoundwa na Waziri wa Mambo wa Ndani, Dk. Emmanuel Nchimbi, kwa maelezo kuwa inaongozwa na jaji asiye na sifa.
Kimesema kuwa Jaji huyo mstaafu, Stephen Ihema, anafahamika ni mtu asiyejua kazi, kwani ameshindwa kutoa hukumu katika kesi zaidi ya 300.
Akizungumza na waandishi jana jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Masuala ya Sheria, Katiba na Haki za Binadamu wa chama hicho, Tundu Lissu, alisema kutokana na Jaji Ihema kutoweza kazi, hata Jaji Bernard Luanda alipata kumkosoa kwa kutoa waraka kwa majaji wote mwaka 2005.
“Kama mnafuatilia taarifa za hivi karibuni, Ihema ni mmoja wa majaji waliopo kinyume cha sheria na Katiba. Aliteuliwa kuwa jaji enzi za Benjamin Mkapa, ilipofika mwaka 2003 kwa sababu hakuwa anajua sheria,” alisema.
Lissu ambaye ni Mbunge wa Singida Mashariki, aliongeza kuwa Ihema hajui kazi ya ujaji na kwamba alisharundika zaidi ya kesi 300 ambazo anashindwa kuziandikia hukumu. Na kuwa mtu ambaye anajulikana kutokuwa na uwezo wowote wa kufanya kazi ya kisheria.
“Ndugu zangu na hili naomba nirudie maana wasiseme tumeanza maneno yetu, mwaka 2003 kabla mimi sijawa mbunge kuna mtu anaitwa Joram Alute, ni Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa wa Singida kwa sababu ya ubovu wa Jaji Ihema, Joram alimwandikia Rais Mkapa barua ya kumuomba kumuondoa Jaji Ihema Mahakama Kuu, kwa sababu hakuwa na uwezo wowote wa kufanya kazi ya ujaji.
Miaka karibu 10 wana CCM, Joram Alute, si CHADEMA, alisema hawezi kazi, aidha ni mvivu au hajui namna ya kuandika hukumu, hafai kuwa jaji,” alisema Lissu.
Aliongeza kuwa mwaka 2005 Jaji Ihema alikuwa amemaliza mkataba wa kwanza na kupewa mwingine wa kazi ya ujaji, hali ambayo ilimfanya Jaji Bernard Luanda (sasa Jaji wa Mahakama ya Rufaa), baada ya kuandikiwa na Jaji Manento kuwa Ihema amepewa mkataba wa ujaji, aliandika waraka uliosambazwa kwa majaji wote kuwa Ihema si jaji kwa mujibu wa Katiba.
Alisema kwa mujibu wa sheria za nchi, majaji wanateuliwa, hivyo Jaji Ihema kupewa mkataba ni kinyume cha sheria na katiba.
Lissu alieleza kuwa hata alipopelekwa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma, tume hiyo ilikuwa ni ya kuficha uchafu na madhambi ya viongozi, kwani ilikuwa kimya kwa miaka yote huku viongozi wakishiriki kufilisi taifa.
Alisema kutokana na maelezo hayo ni dhahiri kuwa Ihema hana uwezo na pia maadili yake ni ya mashaka, kwani hilo linafahamika ndani ya mahakama.
Pamoja na hilo, alisema tume hiyo imeundwa kwa lengo la kurekebisha mambo baada ya Jeshi la Polisi kukamatwa mchana kweupe wakifanya mauaji.
“Ni tume ambayo lengo lake si kuchunguza mauaji, ni kuondoa hii picha ya mauaji yaliyofanywa na Jeshi la Polisi hadhaharani…hii ndivyo tunavyoiangalia.
Kwa kuwa si tume ya kuchunguza mauaji sisi kama chama hatutaiunga mkono na tutawashauri wananchi wa Tanzania, wawe wanachama wetu, wasiwe wanachama wetu, wasiiunge mkono,” alisema.
Nchimbi akosolewa
Lissu alisema kwa mujibu wa sheria ya kuunda tume za uchunguzi mwaka 1962 sura ya 29, anayepaswa kuunda tume ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kutoa hadidu rejea na kwamba kulingana na utaratibu huo si jukumu la waziri kuunda tume.
Alisema tume za aina hiyo zinatoa ripoti kwa rais au zinaweza kutoa taarifa hadharani endapo rais ataelekeza hivyo katika hadidu rejea.
“Hivyo kwa matukio makubwa ya kitaifa yanayotokea, kisheria ni jukumu la rais, si jukumu la waziri ambaye anawasimamia watuhumiwa wa hicho kinachotakiwa kuchunguzwa.
Kwa hiyo katika upeo huo wa kisheria, Waziri Nchimbi hana mamlaka ya kuunda tume ya kuchunguza mauaji hayo,” alisema.
Lissu alifafanua kuwa walioua ni polisi ambao inawezekana waliamriwa waue na wakubwa zao kisiasa (waziri) au kiutendaji (IGP na maofisa wengine wa jeshi), hivyo kama unachunguza mauaji yaliyofanyika waziwazi, inawezekana yamefanywa kwa amri za kisiasa au kiutendaji.
Hivyo alihoji kama tume hiyo ina uwezo wa kumhoji waziri au IGP na kusema kuwa: “Tume hii ni danganya toto, ya kitchen party, pengine na ya marafiki, ili kuondoa picha mbaya kwa Jeshi la Polisi,” alisema.
Wajumbe wake waguswa
Lissu alisema Naibu Kamishna wa Polisi, Isaya Mungulu, kutoka makao makuu hana uwezo kwa kumuita waziri au IGP kwa ajili ya kumhoji kuhusiana na mauaji hayo.
Kuhusu mtaalamu wa mabomu, Wema Wapo, kutoka Jeshi la Ulinzi wa Wananchi wa Tanzania (JWTZ) alihoji kuwa anakwenda kuchunguza kitu gani kisichojulikana, kwani katika picha muuaji anajulikana.
“Inaonekana ni bomu la machozi ambalo alipigwa nalo, ambalo limemchanachana. Sasa ni kitu gani kisichojulikana. Sasa unaita mtaalamu achunguze mlipuko upi ambao haujulikani?” alihoji.
Kwa upande wa Theopili Makunga kutoka Jukwaa la Wahariri (TEF) na Pili Mtambalike kutoka Baraza la Habari Tanzania (MCT), alisema hao ni waandishi wa habari na kuhoji iwapo wana utaalamu wa kuchunguza vifo.
“Hii ni tume ya marafiki, yenye lengo la kukosha mauaji yaliyofanywa na marafiki, kwa vyovyote vile hii si tume halali ya kuchunguza mauaji ya Mwangosi,” alisema Lissu.
Hadidu rejea zapingwa
Lissu alihoji ni mtu gani asiyefahamu chanzo cha mauaji hayo, kwani vyombo vya habari vimemuonyesha kupitia picha, hivyo kuhoji tume hiyo inakwenda kuchunguza kitu gani.
Kuhusu swali kama kweli kuna uhasama kati ya polisi mkoani Iringa na waandishi, alihoji iwapo tume hiyo inakwenda kuchunguza mauaji ama uhasama.
Kwa upande wa swali kama nguvu iliyotumika na polisi ilikuwa sahihi, alisema kuwa hilo ni suala la kisheria na pia kunahitajika ushahidi.
“Kuhusu swali linalohoji mahusiano kati ya polisi na vyama vya siasa. Hili liko wazi kabisa kwa sababu sijawahi kusikia Jeshi la Polisi limevunja mikutano ya CCM, kwa hiyo hapa wanakwenda kuichunguza CHADEMA,” alisema.
Aliongeza kuwa iwapo wanataka kuchunguza suala hilo kwa nini Mungulu yupo kwenye tume hiyo na hakuna mtu wa CHADEMA wala Msajili wa Vyama vya Siasa au mwakilishi wake.
“Hii si tume ya kuchunguza mauaji, ni ya kufunika mauaji haya…hatuwezi kukubaliana na tume hii,” alisema.
Mbali na hilo, alisema kuna haja ya kuchunguza matukio mbalimbali ya mauaji yaliyotokea hivi karibuni likiwemo la Morogoro, Arusha, Igunga na Arumeru Mashariki.
“Matukio yote haya hayajachunguzwa inavyostahili. Hatutaki mambo yaishe hivi hivi,” alisema.
Mapendekezo yao
Kutokana na hali hiyo, alisema chama hicho kinamtaka Rais Jakaya Kikwete kuunda tume ya uchunguzi wa mauaji ambayo itaongozwa na majaji waadilifu na kwamba itakuwa bora iwapo watatoka Mahakama ya Rufaa na Mahakama Kuu, ambao watafanya uchunguzi wa wazi.
“Katika tume hiyo mashahidi watakuwa wakiitwa hadharani. Tume za aina hii hazipo, lakini kwa mujibu wa sheria Rais anaweza kuunda tume hiyo. Hatutaki uchunguzi wa kificho ambao unaonesha polisi hawakukosea,” alisema.
Alieleza kuwa tume hiyo itakuwa na mamlaka ya kumuita mtu yeyote isipokuwa rais. Na kwamba kwa kuwa muuaji anajulikana, chama hicho kinataka askari wote waliohusika wakamatwe na kufunguliwa kesi ya mauaji.
“Tunajua si wote walioua, ila katika sheria kuna kitu kinaitwa common intension, mmoja ameua, lakini alioshirikiana nao wanahusika. Hili linawezekana kwa kuwa kuna ushahidi,” alisema.
Alisema iwapo rais hataunda tume hiyo, kuna njia nyingi za kuendelea na suala hilo, na kusema hilo chama kinapaswa kutoa kauli.
Wataka Nchimbi ajiuzulu
Katika hatua nyingine, Lissu alisema kutokana na tukio hilo, Waziri Nchimbi anapaswa kuwajibika kisiasa kwa kujiuzulu, kwani hawezi kuendelea kuwa waziri na kuheshimika kutokana na tukio hilo.
“Kama ana chembe ya uadilifu afuate nyayo za Mwinyi (Ali Hassan Mwinyi) miaka 36 iliyopita ambaye alijiuzulu uwaziri. Nchimbi hawezi kuwa waziri na kuendelea kuheshimika kama anaongoza jeshi la wauaji. Akishindwa kujiuzulu rais amfukuze kazi,” alisema.
Alieleza kuwa mauaji ya aina hiyo ni ya kisiasa na kuongeza kuwa jeshi hilo limekuwa likifanya kazi kwa niaba ya CCM.
Tendwa aibuka
Mauaji ya Daudi Mwangosi, anayedaiwa kuuawa kwa bomu na askari polisi mkoani Iringa, yamemuibua Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, John Tendwa, ambaye ametishia kuvifuta vyama vinavyojihusisha na siasa za vurugu.
Katika mkutano wake na waandishi wa habari jana, Tendwa ambaye alitumia muda mwingi kuwatisha CHADEMA pia amelionya Jeshi la Polisi na kulitaka lifanye kazi zake kwa wajibu wa sheria za nchi.
Tendwa ambaye ofisi yake imekuwa ikilalamikiwa na vyama vya upinzani kuwa inashindwa kutekeleza wajibu wake kutokana na kuegemea upande wa Chama tawala cha CCM, alisema kuwa demokrasia ya sasa imekua na kusababisha vifo vya raia wasio na hatia.
Alisema hawezi kuvumilia siasa za vurugu zinazohatarisha amani ya taifa lililopata uhuru wake miaka 50 iliyopita kwa kisingizio cha operesheni za ukombozi.
Tendwa alisema haoni haja ya CHADEMA kuendelea na operesheni yao ya Vuguvugu la Mabadiliko (M4C) wakati huu ambao si kipindi cha uchaguzi, hivyo kutishia kukifuta chama hicho alichodai mikutano yake imekuwa ikizusha vurugu.
Aliainisha kuwa kuanzia mwaka jana hadi sasa mauaji kadhaa ya raia yametokea katika mikutano ya kisiasa katika mikoa ya Arusha, Singida, Morogoro na Iringa na kwamba hali hiyo haiwezekani kusema taifa ni huru.
Alisema kuwa Agosti 10 mwaka huu, mkutano wa vyama vya siasa na Jeshi la Polisi ulifanyika na kuzungumzia masuala mbalimbali likiwamo la amani nchini, kufanyika kwa mikutano ya vyama, wajibu wa vyama vya siasa kwa kufuata sheria za nchi na wajibu wa Jeshi la Polisi nchini.
Tendwa aliongeza kuwa kutokana na kuwapo kwa sheria ya mikutano ya vyama vya siasa nchini, ikitokea chama chochote cha siasa kitaleta chuki na uvunjifu wa amani kitapaswa kufutwa.
“Kutokana na hali tuliyoifikia kwa sasa inatisha, hivyo vyama vya siasa viondoe uchochezi,” aliongeza.
Pia amelitaka Jeshi la Polisi kutimiza wajibu wake wa kulinda raia pamoja na mali zao na kuwataka wavitumie vyombo vyao kwa ustaarabu.
DCI asuswa Iringa
Jeshi la Polisi nchini limeanza kuonja shuluba ya matukio yao kususiwa na waandishi wa habari, ambapo jana Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai nchini, DCI Robert Manumba, alikuwa wa kwanza kukumbwa na adha hiyo mkoani Iringa.
Waandishi wa habari wameazimia kutoripoti taarifa zozote za jeshi hilo hadi hapo wale waliohusika katika kusababisha kifo cha mwanahabari, Daudi Mwangosi, watakapokuwa wamekamatwa na kuchukuliwa hatua.
Manumba ambaye jana alikuwa akitaka kutoa taarifa za awali juu ya uchunguzi wa kifo cha Mwangosi, alijikuta katika wakati mgumu baada ya wanahabari hao kugoma kabisa kwenda kumsikiliza.
Pia waandishi hao wamekosoa tume iliyoundwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi, wakisema haijakidhi haja wala kuzingatia uwiano, kwa kile walichoeleza kuwa hakuna hata klabu moja ya waandishi wa habari iliyoshirikishwa.
Awali waandishi hao walitoa masharti kwa DCI wakitaka awepo peke yake katika chumba cha mikutano lakini Manumba alijitetea kuwa tamko alilotaka kutoa ni lazima na maofisa hao walisikie.
“Jamani punguzeni jazba juu ya hili, ninajua mna mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa hili na suala hili limemgusa kila mmoja, hasa ninyi waandishi wa habari, hivyo naomba mnisikilize na mjue tunataka kuwaambia nini,” alisema DCI Manumba bila mafanikio.
Wakati huo huo, waandishi wa habari mkoani hapa, walisema wakati tume iliyoundwa na Dk. Nchimbi haijaanza kazi yake rasmi ni vema Kamanda wa Polisi mkoani humo akaachia madaraka yake kwa muda ili kupisha uchunguzi huru.
Katibu wa Chama cha Waandishi wa Habari Mkoa wa Iringa, Frank Leonard, alisema mbali na kumtaka Kamuhanda kujiuzulu pia ni wakati muafaka kwa tume iliyoundwa ikawahusisha na viongozi wa klabu ya waandishi.
TUCTA yamlilia Mwangosi
Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Nchini (Tucta), limemlia aliyekuwa mwandishi wa kituo cha runinga cha Channel Ten, marehemu Daudi Mwangosi, likisema alikuwa ni mchapa kazi.
Katibu Mkuu wa Tucta, Hezron Kaaya, alisema kuwa ni jambo la kusikitisha na kushangaza kwa mwandishi kuuawa wakati akitekeleza majukumu yake.
“Kwa kweli Tucta kati ya mambo ambayo yametuuma na kutusikitisha ni kifo cha Mwangosi kinachoripotiwa kufanywa na Jeshi la Polisi, hasa kitendo cha kusambaratishwa mwili wake, kwani hata mnyama anapouawa katika mawindo huwa hauawi kwa namna ile,” alisema.
Kaaya aliongeza kuwa ni jambo la kusikitisha kwa kuwa kifo kile kitachukua muda mrefu kwa Watanzania kukisahau kwani hakuwa na kosa lolote alilolifanya mpaka kuuawa namna ile.
Aliongeza kuwa kwa hali ilivyo sasa taifa linaelekea pabaya, kwa sababu haki ya mnyonge haizingatiwi tena na wenye nguvu, akitoa mfano kuwa wanyonge wanapodai haki yao jibu rahisi ni kusambaratishwa kwa mabomu na virungu vya polisi.
Alisema endapo hali hiyo itaachwa iendelee hivyo, kunaweza kutokea maafa makubwa kwa wananchi waliochoka kuonewa na kudhulumiwa haki zao.
Kaaya alibainisha kuwa Watanzania wengi wameuawa katika matukio ya kisiasa na hakuna hatua madhubuti zilizochukuliwa kukomesha hali hiyo isiendelee kutokea, badala yake zinaundwa tume ambazo hata hivyo hazijulikani zinakoishia zaidi ya kutumia fedha za walala hoi.

Tanzania Daima

Chadema UK Ndani ya Milton Keynes

DAR NI SISI - VIDEO MAISHA YA WANADAR HATA BAADA YA MIAKA50 YA UHURU